Sunday, June 30, 2013

HALMASHAURI SIMANJIRO YATUNISHIANA MISULI NA MAMLAKA YA MJI MDOGO MIRERANI, DIWANI NYARI AAPA MAMLAKA HIYO IKIFA ATAJIUZULU

 MANYARA
Na Mwandishi wetu, Tanzaniasasa,


MGOGORO Mkubwa umeibuka kati ya Halmashauri ya Wilaya ya  Simanjiro na uongozi wa mamlaka ya mji mdogo Mirerani wilayani humo baada ya mamlaka hiyo kutangaza msimamo mgumu wa kuzuia watendaji wa Halmashauri hiyo kukusanya mapato ndani ya mji huo na badala yake wao ndio watafanyakazi hiyo.

Adha wajumbe wa mamlaka hiyo wameitaka Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro kuwataka radhi wajumbe hao kwa madai ya kuwakashifu kwa kuwaita ‘bado watoto wadogo’ kupitia barua waliomuandikia mtendaji mkuu wa mamlaka hiyo baada ya wao kuitaka Halmashauri hiyo kusitisha zoezi la kukusanya mapato ndani ya mji wao.

Uamuzi huo mgumu ulifikiwa jana katika kikao cha wajumbe wanaounda baraza la mamlaka ya mji mdogo wa Mirerani chini ya mwenyekiti wake Albert Siloli ambao kwa pamoja walimtaka Mtendaji Mkuu wa mamlaka hiyo ya mji mdogo  kuiandikia barua Halmashauri kuhusu uamuzi huo walioufikia.

Wajumbe hao walikubaliana kuanza zoezi la kukusanya mapato hayo leo (Julai mosi, 2013), ambapo watatawanyika katika maeneo mbalimbali ya mji huo mdogo wa mirerani na fedha watakazozikusanya wataziweka benki kwa ajili  ya utekelezaji wa shughuli za maendeleo zinazohusu mji huo.

Diwani wa viti maalum kupitia kata ya Mirerani Rahel Kinaliki akichangia katika kikao hicho baada ya kutuhumiwa kuihujumu mamlaka hiyo, lakini hata hivyo alikanusha na kusema yuko pamoja na wajumbe wengine kuzuia mapato hayo kukusanywa na watendaji wa Halmashauri
Hata hivyo akizungumzia suala hilo, Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Brigedia Jenerali Francis Kayombo alikiri kuwepo kwa mgogoro huo lakini alisema bado Halmashauri ya Wilaya ndio yenye mamlaka ya kukusanya mapato katika eneo hilo kufuatia kuwa na watendaji wa kuweza kusimamia mapato hayo.

“ Mgogoro huu naufahamu lakini hii mamlaka bado ni ndogo sana na haina watumishi  wa kutosha, haina mwekahazina ambae atakuwa na jukumu la kusimamia mapato watakayokusanya lakini zaidi watazihifadhi wapi hizo fedha wapi?, naomba unisubiri mpaka nirudi kutoka safarini nitawapatia taarifa nzuri zaidi,”alisema.

Afisa mtendaji mkuu wa Mamlaka hiyo ya mji mdogo Mirerani, Nelson Msangi alisema mji huo wenye wakazi zaidi ya elfu54 unatakiwa kupokea ruzuku ya milioni 30 kwa mwaka kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro lakini wamekuwa hawapati fedha hizo na kushindwa kulipa madeni inayodaiwa.

Vyanzo vya mapato hayo ni pamoja na ushuru wa stendi ya mabasi mirerani, machinjio, soko, mnada, hoteli, saluni, nyumba za kulala wageni, kodi ya mabango, leseni za vileo na leseni za biashara ambavyo kwa kipindi cha miaka minne toka 2008 eneo hilo lilipopewa hadhi ya mamlaka ya mji mdogo bado halmashauri hiyo ndio imekuwa ikikusanya.

Wakati huo huo Diwani wa kata ya Mirerani na mjumbe wa baraza hilo Justine Nyari amesema endapo Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro itaifuta mamlaka hiyo atakuwa tayari kujiuzulu wadhifa wake wa udiwani kwa kile alichodaiwa itakuwa ni kuihujumu mamlaka hiyo.


Gari la kubeba uchafu ililokabidhiwa mamlaka ya mji mdogo Mirerani, hata hivyo gari hilo ni bovu

Mwenyekiti wa Mamlaka ya mji mdogo wa Mirerani Albert Siloli akifungua kikao hicho cha baraza la mamlaka ya mji mdogo Mirerani

Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya mji mdogo Mirerani Nelson Msangi akisoma moja ya barua zilizotoka Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro

Diwani wa kata ya Mirerani Justine Nyari akichangia hoja ya kuizuia Halmashauri ya wilaya ya Simanjiro kuendelea kukusanya mapato katika mamlaka ya mji mdogo Mirerani leo

mmoja wa wajumbe wa baraza la mamlaka ya mji mdogo Mirerani akichangia hoja katika kikao hicho

Friday, June 28, 2013

ASKOFU MKUU INTERNATIONAL EVANGELISM AKEMEA WANASIASA WANAOPINGA SERIKALI ILIYOPO MADARAKANI



Askofu Issangya akihubiria

Na Mwandishi Wetu, Tanzaniasasablog

ASKOFU mkuu wa kanisa la International Evangelism Center (IEC), Sakila Eliud Issangya amewataka wanasiasa wanaopinga Serikali iliyoko madarakani kuacha mara moja kwa kuwa imechaguliwa kisheria.

Akihutubia maelfu ya waumini wa kanisa hilo jana katika maadhimisho ya
miaka 30 ya kuanzishwa kwa chuo cha Biblia chini ya kanisa hilo
Issangya alisema katika siku za hivi karibuni kumekuwepo na vuguvugu
la vijana na wanasiasa kutoheshimu mamlaka iliyopo nchini.

Alisema kutii mamlaka iliyopo sio ombi ni suala la lazima kwa kuwa
imechaguliwa kihalali na wananchi hivyo endapo wapo wanaofikiri haifai
wasubiri muda ukifika watumie haki yao ya kupiga kura na kuchagua
viongozi wanaowataka wao.

“Biblia inasema tuheshimu mamlaka zetu, kutiii mamlaka iliyopo sio
ombi maana usipoheshimu na wewe hutoheshimiwa hivyo serikali iliyopo
ni lazima uiheshimu kwani ni sawa na Baba na Mama yako, ukitaka
kutawala huwezi kutawala Baba na Mama yako labda usubiri mpaka
wafe,”alisema Issangya.

Alisema kuwa vuguvugu la kutoheshimu mamlaka iliyopo madarakani
imekuwa ikichangiwa kwa sehemu kubwa na vijana ambao mawazo yao
yamekuwa na moto ambao unatakiwa kutulizwa na wazee kwa kuwafunza
masuala ya uongozi ili wawe viongozi bora.

Askofu Issangya akihubiria

Askofu Issangya akihubiria maelfu ya waumini wa kanisa hilo

Askofu Issangya akitambulisha watoto wake na hapa anamtambulisha Alaine mmoja wa watoto wake ambae anatarajia kufunga ndoa mapema mwezi ujao

Mke wa Askofu Issangya akisalimia waumini

Askofu Mkuu Eliud Issangya akiwa amekabidhiwa kesi ya birthday ya miaka 30 kuanzishwa kwa chuo cha biblia


Mchungaji Mansah akigawa vitabu vyenye historia ya miaka 30 ya kuanzishwa kwa chuo hicho

Waumini wakisikiliza kwa makini

Mmoja wa wanzilishi na mfadhili wa chuo hicho shirley Bedsole akiimba wimbo katika jubilee hiyo

wachungaji wa kanisa hilo kutoka barani Afrika wakiingia kanisani kwa maandamano

kwaya ya kanisa la International Evangelism Sakila ikitumbuiza

BARAZA LA HABARI LAKUTANA NA WANAFUNZI AJTC, LATOA ONYO KWA WAHARIRI, WAANDISHI, WATAKIWA KUFUATA WELEDI KATIKA KUANDIKA HABARI ZAO



Na Mwandishi wetu, Tanzaniasasa

WAKUFUNZI wa vyuo vinavyotoa elimu ya uandishi wa habari nchini wametakiwa kuwafundisha kwa ufasaha wanafunzi wao maudhui yaliyopo katika azimio Dar es salaam kuhusu uwajibikaji na uhuru wa vyombo vya habari (DEFIR), ili kutengeneza waandishi watakaofuata maadili ya habari na kuwa kioo kwa jamii.

Wito huo umetolea leo jijini hapa na Meneja utafiti na machapisho wa Baraza la Habari nchini (MCT),  John Mirenyi katika warsha ya siku moja kuhusu azimio hilo kwa wakufunzi na wanafunzi wa chuo cha uandishi wa habari Arusha (AJTC).



wanafunzi wa chuo cha uandishi wa habari Arusha, wakisoma maswali ya tathmini ya warsha hiyo , picha na seif mangwangi wa tanzaniasasablog

Mirenyi amesema taaluma ya habari imekuwa ikipokea waandishi wengi kila siku jambo ambalo limekuwa likisababisha baadhi yao kuvunja maadili ya uandishi wa habari na kuifanya kutoheshimiwa na jamii.

Amesema azimio la  Dar es salaam kwa wahariri , waandishi na wamiliki wa vyombo vya habari (DEFIR) limetoa mwongozo wa namna ambavyo waandishi wa habari wanatakiwa kufanya shughuli zao ili kuijengea hadhi taaluma hiyo mbele ya jamii na kuifanya kuheshimika kama zilivyo taaluma zingine.


Mwandishi Mkongwe na Rais wa chama cha waandishi wa habari za mazingira JET Christom Rweyemam akitoa mada kuhusu azimio la wahariri jijini Dar es salaam (DEFIR) katika semina hiyo

Mwandishi Mkongwe na Rais wa chama cha waandishi wa habari za mazingira JET Christom Rweyemam akitoa mada kuhusu azimio la wahariri jijini Dar es salaam (DEFIR) katika semina hiyo

Wakisikiliza kwa makini

John Mirenyi Meneja utafiti na machapisho wa Baraza la Habari Tanzania (MCT0, akimtambulisha mmoja wa waandaaji wa semina hiyo ambae pia ni mwanafunzi wa chuo cha uandishi wa habari Arusha

Wakimsikiliza kwa makini mtoa mada

Wanafunzi wa chuo cha uandishi wa habari Arusha AIJTC wakimsikiliza kwa makini mtoa mada (hayupo pichani).

Wakufunzi na wanafunzi wa chuo cha uandishi wa habari Arusha, wakisoma maswali ya tathmini ya warsha hiyo , picha na seif mangwangi wa tanzaniasasablog

Mhariri wa Radio Safina  Lucas Daniel  akisaini azimio la DEFIR