Monday, July 22, 2013

WILAYA YA HAI YAINGIA USHIRIKIANO WA MAENDELEO NA SWEDEN

Meya wa manispaa ya Arvidsjaur,Jerry Johqnsson(Katikati) akifafanua jambo baada ya kumalizika itifika ya kusaini makubaliano na hamashauri ya wilaya ya Hai,anayeshuhudia ni mwenyekiti wa halmashauri Clement Kwayu

Viongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Hai na wale wa Manispaa ya Arvidsjaur katika kusainiana makubaliano ya ushirikiano

Watendaji wa Manispaa ya Arvidsjaur na halmashauri ya wilaya ya Hai wakibadilishana mkataba wa ushirikiano

Mratibu wa mipango ya maendeleo ambaye pia ni diwani katika manispaa ya Arvidsjaur,Stina Johansson(tatu Kulia) akiwa na ujumbe wa viongozi kutoka wilayani Hai-kutoka kulia,Novats Makunga(Mkuu wa wilaya),Clement Kwayu(Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya),Melkizedeck Humbe(Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri) na Ester Mbatiani ambaye ni afisa mipango mkuu wa Halmashauri
Na Richard Mwangulube,Hai


Halmashauri ya wilaya ya Hai,imeingia mkataba wa miaka minne wa ushirikiano na Manispaa ya Arvidsjaur  nchini  Sweden  unaolenga katika maeneo ya kiuchumi na kijamii ukiwemo wa teknolojia ya kisasa ya udhibiti wa takataka kiuchumi kwa kuziwezesha kutengezwa upya bidhaa kwa ajili ya matumizi.

Mkataba huo ulitiwa saini  wakati wa ziara ya ujumbe wa viongozi  wa wilaya ya  Hai uliyoongozwa na Mkuu wa Wilaya Hiyo, Novatus Makunga hivi karibuni katika  makao Makuu ya Manispaa hiyo nchini Sweden.

Wajumbe wengine Katika ziara hiyo ya siku tano ambao ndiyo waliosaini mkataba huo ni pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri  ya Wilaya ya Hai Clement Kwayu, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Melkizedeck Humbe pamoja na Afisa Mipango   wa Halmashauri Ester Mbatian.

Kufuatia  mkataba huo, Halmashauri ya Wilaya ya Hai itapaswa  kuandaa na kuwasilisha katika Manispaa ya Arvidsjaur  miradi mbalimbali inayolenga katika Nyanja za biashara na  viwanda vidogo na vya kati.

Maeneo mengine ya shirikiano huo ni pamoja na  elimu na utoaji wa taarifa, uboreshaji   na usimamizi  wa mazingira endelevu pamoja na miradi inayolenga   masuala ya  ajira  kwa vijana.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Hai mwishoni mwa wiki,Makunga  amesema kadhalika ushirikiano ho unalenga  katika kuimarisha  shughuli  mbalimbali zinazohusiana na masuala ya sekta ya utalii na utawala bora kuanzia ngazi ya chini kabisa.

“Kwa kushirikiana na wenzetu tunaandaa mkakati wa kuimarisha mafunzo kwa  jamii katika masuala ya uchumi na  shughuli za maendeleo ya Kijamii na lengo kubwa zaidi ni kwa kundi la vijana”. Amefafanua Makunga.

Ameeleza kupitia Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Sweden[SIDA] ushirikiano huo pia   utatoa fursa kwa Manispaa ya Arvidsjaur kushirikiana na wilaya ya Hai katika ujenga uwezo kwa halmashauri juu ya namna ya kupata taarifa mbalmbali za maendeleo  na kiuchumi kutoka maeneo ya vijijini nakuzifanyia kazi.

Amesema pia ushirikiano huo umelenga katika kuhakikisha halmashauri ya Hai inaingia katika mfumo wa kisasa wa namna ya kusimamia  ukusanyaji wa mapato na matumizi ya fedha za maendeleo, kuboresha mawasiliano na wadau mbalimbali  ikiwemo kupitia kituo cha halmashauri hiyo cha redio  Boma FM.

Amesemasa Manispaa  hiyo ya Sweden  itasaidia  katika ujenzi,uboreshaji na uendelezaji wa  kituo cha  mafunzo kwa ajili ya  maendeleo ya jamii katika wilayani Hai pamoja na kusaidia  katika kuboresha huduma za afya.

Masuala mengine yatakayotekelezwa  kutokana na mahusiano hayo  ni pamoja na Manispaa ya Arvidsjaur kusaidia katika teknolojia ya urudufishaji wa taka ambapo unawezesha taka ngumu na taka maji kuweza kutumika tena.

Makunga amesema kuwa suala la udhibiti wa takataka ni changamoto kubwa katika mji wa Hai ambao hauna dampo huku kukabiliwa na ongezeko la kasi la watu wanaopenda kuweka makazi ya kuishi na kuendesha shughuli zao za kazi Arusha,Moshi,Siha na Simanjiro.

“Kwa wenzetu taka ni rasilimali, inachambuliwa kuanzia ngazi ya familia na kupelekwa eneo la kutupa taka, kwa kupangwa kuangalia na aina, na hutumika kutengeneza bidhaa mbalimbali vikiwemo vikombe, vijiko, sahani na umeme pamoja na mafuta ya kulainishia vyuma kutumika upya,”amefafanua.

Ametaja mengine ambayo yatatiliwa mkazo kutokana na ushirikiano huo ni pamoja na  Manispaa hiyo kusaidia katika kukuza uchumi na kuimarisha miundo mbinu ya kiuchumi.

Makunga ameeleza kuwa manispaa hiyo ambayo inamiliki uwanja wa ndege wa kimataifa imeonyesha kuvutiwa kusaidia uimarishaji wa  uwanja wa kimataifa wa Kilimanjaro(KIA)  uliopo wilayani Hai kwa kuongeza  shughuli za  biashara za Anga pamoja na kuboresha miundo mbinu katika Uwanja huo.

Ujumbe huo uliweza kupata taarifa juu ya shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Manispaa hiyo zikiwemo za kuchumi, kijamii pamoja na usimamizi bora  wa ukusanyaji na matumizi ya Mapato.

Kwa mujibu wa nchi ya Sweden, Mamlaka zote  za Serikali za Mitaa zinajulikana kama Manispaa zinaongozwa kwa sheria ya bunge la nchi hiyo ambapo hivi sasa kuna Manispaa zipatazo 260 nchini Sweden
 
Manispaa hizi zinawajib wa kusimamia  masuala ya  elimu kuanzia ngazi ya chekechea hadi Sekondari pamoja na kujenga na kusimamia vituo vya malezi ya  wazee na wasiojiweza.

Kadhalika manispaa hizi zinawajibu wa  kusimamia vituo vya zimamoto na uokoaji,kusimamia ujenzi  na uendeshaji  wa viwanja vya ndege,kusaidia walemavu pamoja na kuunganisha wajiri na waajiriwa

Pia Makunga ameeleza kuwa Manispaa hizi zinajukumu la kusimamia vituo vya  elimu ya ujasirimali kwa vijana na masuala ya Utalii ambapo  Sweden kila siku hupokea watalii zaidiya 500,000 wanaotembelea vivutio mbalimbali katika Manispaa hizo kutoka nchi za ulaya.

No comments: